Loading...
Larger font
Smaller font
Copy
Print
Contents
  • Results
  • Related
  • Featured
No results found for: "".
  • Weighted Relevancy
  • Content Sequence
  • Relevancy
  • Earliest First
  • Latest First
    Larger font
    Smaller font
    Copy
    Print
    Contents

    Siri ya Uovu

    Katika barua ya pili kwa Wathesalonike, mtume Paulo alitabiri uasi mkuu ambao ungekuwa na matokeo ya kuanzishwa kwa mamlaka ya upapa. Alitangaza kuwa siku ya Kristo isingekuja “usipokuja kwanza ule ukengeufu; akafunuliwa yule mtu wa kuasi, mwana wa uharibifu; yule mpingamizi, ajiinuaye nafsi yake juu ya kila kiitwacho Mungu ama kuabudiwa; hata yeye mwenyewe kuketi katika hekalu la Mungu, akijionyesha nafsi yake kana kwamba yeye ndiye Mungu.” Na zaidi, mtume huyu anawaonya waumini wenzake kuwa “ile siri ya kuasi hivi sasa inatenda kazi.” 2Wathesalonike 2:3,4, 7. Hata katika muda ule wa miaka ya awali aliona, yakilinyemelea kanisa, makosa yale ambayo yangeandaa njia kwa ajili ya kujitokeza kwa Upapa.PLK 112.2

    Kidogo kidogo, mwanzoni kwa siri na kimya kimya na kisha kwa uwazi zaidi kadiri ilivyozidi katika nguvu na kupata udhibiti wa akili za wanadamu, siri ya uovu ilitenda kazi yake ya udanganyifu na kufuru. Karibu bila kutambuliwa desturi za upagani ziliingia katika kanisa la Kikristo. Roho ya mapatano na makubaliano iliachwa kwa muda ili kupisha mateso makali ambayo kanisa lilistahimili chini ya upagani. Lakini mateso yalipokoma, na Ukristo kuingia katika viwanja na ikulu za wafalme, uliweka kando usahili wa unyenyekevu wa Kristo na mitume na kutwaa majivuno na kiburi cha makuhani na watawala wa kipagani, na mahali pa matakwa ya Mungu uliweka nadharia na mapokeo ya wanadamu. Uongofu wa jina tu wa Kostantino katika sehemu ya awali ya kame ya nne ulisababisha furaha kuu, na dunia, ikiwa imevikwa mavazi ya haki, ilitembea kuingia kanisani. Sasa kazi ya uharibifu iliendelea kwa kasi. Upagani, ukiwa unaonekana kushindwa, ulikuwa ndio mshindi. Roho yake ilitawala kanisa. Mafundisho yake, taratibu za ibada, na ushirikina wake vilijumuishwa katika imani na ibada ya waliokiri kuwa wafuasi wa Kristo.PLK 112.3

    Maridhiano haya kati ya upagani na Ukristo yalikuwa na matokeo ya kujitokeza kwa mtu wa kuasi aliyetabiriwa katika unabii kuwa anapinga na kujiinua juu ya Mungu. Mfumo ule mkubwa wa dini ya uongo ni kazi ya mikono ya uwezo wa Shetani-ukumbusho wa juhudi zake za kujiweka mwenyewe katika kiti cha enzi na kuitawala dunia kulingana na mapenzi yake.PLK 113.1

    Moja ya mafundisho yanayoongoza ya Urumi ni kwamba papa ni kiongozi anayeonekana wa kanisa la Kristo ulimwenguni mwote, akiwa amevikwa madaraka ya juu kabisa juu ya makasisi na wachungaji katika sehemu zote za dunia. Zaidi ya hili, papa amejichukulia na kujiita majina halisi ya Mungu.PLK 113.2

    Shetani alijua vyema kuwa Maandiko Mataka- tifu yangewawezesha watu kutambua udanganyifu wake na hivyo kuhimili uwezo wake. Ilikuwa ni kwa Neno ambapo hata Mwokozi wa ulimwengu aliweza kupinga mashambulizi yake. Katika kila shambulio Kristo aliwasilisha ngao ya ukweli wa milele, akisema, “Imeandikwa.” Kwa kila pendekezo la adui alijibu kwa hekima na uwezo wa Neno. Ili Shetani adumishe ushawishi wake kwa watu na kujitwalia mamlaka ya kipapa bila haki, ni lazima awaweke katika ujinga wa kutoyaelewa Maandiko. Biblia ingemtukuza Mungu na kuwaweka wanaume na wanawake wenye ukomo katika nafasi yao stahili. Kwa sababu hii, kweli zake takatifu ni lazima zifichwe na kukomeshwa. Mantiki hii ilikubaliwa na kanisa la Kirumi. Kwa miaka mamia lilipiga marufuku usambazaji wa Biblia. Watu walikatazwa kuisoma au kuwa nayo katika nyumba zao, na makasisi na maaskofu wapotovu walitafsiri mafundisho yake ili kulinda madai yao. Kwa njia hii papa alitokea kuonekana kana kuwa anakubalika karibia ulimwenguni kote kama naibu wa Mungu duniani, ambaye amepewa mamlaka ya juu kabisa juu ya kanisa na serikali.PLK 113.3

    Kubadilishwa Sheria na Nyakati - Baada ya kuondolewa kigundua makosa, Shetani alitenda kama apendavyo. Unabii ulitangaza kuwa upapa ungekusudia “kubadili majira na sheria” Danieli 7:25. Kazi hii hakuchelewa kuijaribu. Ili kuwapa waongofu kutoka katika upagani kitu mbadala cha kuabudu sanamu, na hivyo kukuza ukubali wao wa Ukristo kijina tu, ibada ya kuabudu sanamu na kumbukumbu za watakatifu wa zamani ziliingizwa polepole katika ibada ya Kikristo. Amri ya baraza kuu hatimaye ilithibitisha mfumo huu wa ibada ya sanamu. Katika kukamilisha kazi hii ovu, Rumi ilithubutu kufuta kutoka katika sheria ya Mungu amri ya pili, ambayo inakataza ibada ya sanamu, na kuigawanya amri ya kumi, ili kudumisha idadi.PLK 114.1

    Roho ya maridhiano na upagani ilifungua njia kwa ajili yakuidharau zaidi mamlakaya Mbingu. Shetani aliigeuza amri ya nne pia, na kukusudia kuiweka kando Sabato ya awali, siku ambayo Mungu aliibariki na kuitakasa, na badala yake kuitukuza siku kuu iliyoshehenekewa na wapagani kama “siku ya kuheshimiwa ya jua.” Badiliko hili mwanzoni halikujaribiwa waziwazi. Katika kame za awali Wakristo wote waliitunza Sabato ya kweli. Walikuwa na wivu kwa ajili ya heshima ya Mungu, na, huku wakiamini kuwa sheria yake haibadiliki, kwa bidii walitunza utakatifu wa maagizo yake. Lakini Shetani alitenda kwa werevu mno kupitia kwa wakala wake ili kutimiza kusudi lake. Ili kuelekeza macho na fikra za watu juu ya Jumapili, ilifanywa kuwa sikukuu kwa ajili ya heshima ya ufufuko wa Kristo. Huduma za kidini zilifanyika katika siku hii, lakini tena ilichukuliwa kuwa siku ya mapumziko, na Sabato bado ilitunzwa kwa utakatifu.PLK 114.2

    Wakati ambapo alikuwa bado mpagani, Konstantino alitoa amri iliyoelekeza utunzaji wa Jumapili kama sikukuu ya taifa katika Himaya yote ya Kirumi. Baada ya uongofu wake alibaki kuwa mtetezi mkuu wa Jumapili, na ndipo aliposhurutisha utiifu wa amri yake ya kipagani kwa ajili ya maslahi ya imani yake mpya. Lakini heshima iliyopewa siku hii bado haikutosheleza kwa wakati ule kuwazuia Wakristo kuiheshimu Sabato ya kweli kuwa takatifu kama alivyo Bwana. Hatua nyingine lazima ichukuliwe: sabato ya uongo lazima iinuliwe kuwa sawa na ile ya kweli. Miaka michache baada ya Konstantino kutoa amri yake, Askofu wa Rumi aliipa jina Jumapili na kuiita siku ya Bwana. Kwa njia hii pole pole watu walianza kuiona kuwa ilikuwa na kiwango fulani cha utakatifu. Lakini bado Sabato ya mwanzo ilitunzwa.PLK 115.1

    Mdanganyifu mkuu alikuwa bado hajakamilisha kazi yake. Alidhamiria kuuweka ulimwengu wa Kikristo chini ya bendera yake na kutumia uwezo wake kupitia kwa naibu wake, papa mwenye kujisifu aliyedai kuwa ni mwakilishi wa Kristo.Kupitia kwa wapagani walioongoka nusunusu, maaskofu wenye tamaa ya makuu, na washiriki wa kanisa wenye kuipenda dunia alikamilisha kusudi lake. Mara kwa mara mabaraza makuu yalifanyika, ambapo watu wenye vyeo kanisani walikusanyika kutoka duniani kote. Karibu katika kila baraza Sabato ambayo Mungu aliianzisha ilikandamizwa chini kidogo wakati Jumapili ilitukuzwa kwa kiwango hicho hicho. Hivi ndivyo ambavyo sikukuu ya kipagani hatimaye ilikuja kuheshimiwa kama taasisi ya Mungu na huku Sabato ya Biblia ilitangazwa kuwa kumbusho la dini ya Kiyahudi, na watunzaji wake wakatangazwa kuwa wamelaaniwa.PLK 115.2

    Mwasi mkuu alifanikiwa katika kujiinua nafsi yake “juu ya kila kiitwacho Mungu ama kuabudiwa.” 2 Wathesalonike 2:4. Alithubutu kuibadili amri pekee ya sheria ya Mungu ambayo kwa dhahiri inawaelekeza wanadamu wote kwa Mungu wa kweli aliye hai. Katika amri ya nne Mungu anadhihirishwa kama Mwumbaji wa mbingu na nchi, jambo linalomtofautisha na miungu yote ya uongo. Ilikuwa ni kwa ajili ya kuwa ukumbusho wa kazi ya uumbaji ndio maana siku ya saba ilitakaswa kama siku ya pumziko kwa ajili ya mwanadamu. Ilikusudiwa daima kumweka Mungu aliye hai akilini mwa wanadamu kama chimbuko la kila kitu na lengo la kicho na ibada. Shetani anajaribu kuwaondoa watu kutoka katika kuwajibika kwao kwa Mungu na kutoka katika utii wa sheria yake. Kwa hiyo anaelekeza juhudi zake mahususi dhidi ya amri moja ambayo inaelekeza kwa Mungu kama Mwumbaji.PLK 116.1

    Waprotestanti kwa sasa wanasisitiza kuwa kufufuka kwa Yesu katika siku ya Jumapili kuliifanya kuwa Sabato ya Wakristo. Lakini ushahidi wa Maandiko unakosekana. Si mitume wala Kristo walio ipa heshima kama hiyo siku ya kwanza ya juma. Utunzaji wa Jumapili kama taasisi ya Kikristo ina chimbuko lake katika ile “siri ya kuasi” ambayo ilianza kazi yake hata katika siku za Paulo. Ni lini na wapi Bwana alimuasili huyu mtoto Upapa? Ni sababu zipi za kweli zinaweza kutolewa kwa ajili ya badiliko ambalo juu yake Maandiko yamenyamaza kimya?PLK 116.2

    Katika kame ya sita Upapa ulikuwa umeimarika. Kiti chake cha utawala kilijikita katika majiji makubwa, na Askofu wa Rumi alitangazwa kuwa kiongozi wa kanisa lote. Upagani ulitoa nafasi kwa Upapa. Joka alikuwa amempa mnyama “nguvu zake na kiti chake cha enzi na uwezo mwingi.” Ufunuo 13:2. Na sasa ilianza miaka 1260 ya ukandamizaji wa kipapa iliyotabiriwa katika unabii wa Danieli na Yohana. (Danieli 7:25; Ufunuo 13:5-7.) Wakristo walilazimishwa kuchagua kati ya kuachia uaminifu wao na kukubali taratibu za kidini na ibada za kipapa, au kupoteza maisha yao katika vyumba vya jela, au kukubali kifo kwa njia ya kitanda cha mateso, moto, au kukatwa kichwa kwa shoka. Sasa yalitimizwa maneno ya Yesu, “Nanyi mtasalitiwa na wazazi wenu, na ndugu zenu, na jamaa zenu, na rafiki zenu, nao watawafisha baadhi yenu. Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu.” Luka 21:16, 17. Mateso dhidi ya waaminifu yalianza kwa hasira kubwa kuliko wakati mwingine wo wote uliotangulia, na dunia iligeuka kuwa uwanja mkubwa wa vita. Kwa miaka mamia kadhaa kanisa la Kristo lilipata kimbilio lake katika upweke na giza. Nabii alisema, “Yule mwanamke akakimbilia nyikani, ambapo ana mahali palipotengenezwa na Mungu, ili wamlishe huko muda wa siku elfu na mia mbili na sitini.” Ufunuo 12:6.PLK 117.1

    Zama za Giza-Kuinuka kwa Kanisa la Kirumi kwenye madaraka kuliashiria mwanzo wa Zama za Giza. Kadiri nguvu zake zilivyoongezeka, giza lilizidi kuwa nene. Imani iliondolewa kutoka kwa Kristo, msingi wa kweli, kwenda kwa papa wa Rumi. Badala ya kumtumainia Mwana wa Mungu kwa ajili ya msamaha wa dhambi na kwa ajili ya wokovu wa milele, watu walimwangalia papa na makasisi na maaskofu ambao aliwapa mamlaka. Walifundishwa kuwa papa ndiye mpatanishi wao, na kwamba hakuna mtu ambaye angeweza kumkaribia Mungu isipokuwa kupitia kwake, na zaidi kwamba alikuwa akisimama mahali pa Mungu kwa ajili yao, na kwa hiyo lazima atiiwe kabisa. Mchepuko kutoka katika masharti yake ilikuwa ni sababu ya kutosha kusababisha adhabu kali mno kutekelezwa katika miili na roho za wakosaji.PLK 117.2

    Kwa hiyo akili za watu ziligeuzwa mbali kutoka kwa Mungu kwenda kwa wanadamu wenye kuweza kutenda makosa, watenda maovu, na wasio na huruma-na zaidi ya hayo, kwa mfalme wa giza mwenyewe, ambaye alitekeleza mamlaka yake kupitia kwao. Dhambi ilivikwa vazi la utauwa. Wakati maandiko yanapokomeshwa, na wanadamu wanafikia kuj ichukulia kuwa wenye mamlaka ya juu kabisa, basi tutegemee ufisadi, udanganyifu, na uovu unaodhalilisha. Sambamba na kuinua sheria na mapokeo ya wanadamu ulikuja uharibifu ule ambao siku zote ni matokeo ya kuweka kando sheria ya Mungu.PLK 118.1

    Siku za Hatari Kubwa -Hizo zilikuwa ni siku za hatari kubwa kwa kanisa la Kristo. Wabeba viwango vya kweli waaminifu walikuwa wachache. Ingawa ukweli haukuachwa bila washuhudiaji, bado kwa nyakati fulani ilielekea kuwa uovu na ushirikina vingekuwa na ushindi kamili, na dini ya kweli ingeondolewa duniani. Kanisa lilisahau injili, lakini desturi za dini ziliongezeka, na watu walilemewa na masharti makali.PLK 118.2

    Walifundishwa siyo tu kumwangalia papa kama mpatanishi wao bali pia kutumainia kazi zao wenyewe kuweza kulipia fidia ya dhambi. Hija za safari ndefii, matendo ya malipizi-kitubio, ibada za kumbusho za watakatifu, ujenzi wa makanisa, mahali patakatifu, madhabahu, ulipaji wa fedha nyingi kwa kanisa-haya na matendo mengine mengi yanayofanana nayo yaliagizwa ili kuepusha hasira ya Mungu au kupata fadhila yake, kana kwamba Mungu alikuwa ni kama wanadamu, kuweza kughadhabishwa na mambo madogo madogo, au kutulizwa kwa zawadi na matendo ya toba!PLK 118.3

    Kame zilizofuata zilishuhudia ongezeko la daima la makosa katika mafundisho yaliyoagizwa kutoka Rumi. Hata kabla ya kuanzishwa kwa Upapa, mafundisho ya wanafalsafa wapagani yalipewa msisitizo na kuleta athari zake kanisani. Wengi waliokiri uongofu bado waling’ang’ania kanuni za falsafa za kipagani, na siyo tu kuendelea kuijifunza bali pia waliisukumiza kwa wengine kama njia ya kupanua mvuto wao kwa wapagani. Hii iliingiza kosa kubwa katika imani ya Kikristo. Kosa lililojitokeza miongoni mwa haya lilikuwa ni imani juu ya kutokufa kwa mtu na kuendelea kwake kuwa na fahamu baada ya kufa. Fundisho hili liliweka msingi ambao juu yake Rumi ilijenga ibada ya kuomba kwa watakatifu, na ibada ya bikira Maria. Kutoka katika hili pia ulichipuka uzushi juu ya mateso ya milele kwa wale wanaokufa bila kutubu, ambao ulijumuishwa mapema katika imani ya kipapa.PLK 119.1

    Mambo haya yaliandaa njia kwa ajili ya kuingiza hila nyingine ya upagani, ambayo Rumi iliita toharani (purgatori), na kuitumia kuwaogofya umati mkubwa uliodanganyika na washirikina. Mafundisho haya ya uongo yalidai kuwapo kwa mahali pa mateso ambapo roho za wale ambao hawakupewa hukumu ya mauti ya milele wangeteseka kwa ajili ya dhambi zao, na ambapo kutoka huko, baada ya kutakaswa uchafu, wanapokelewa mbinguni.PLK 119.2

    Bado uzushi mwingine ulihitajika ili kuiwezesha Rumi kunufaika kutokana na hofu na maovu ya waumini wake. Fundisho la msamaha wa kipapa lilitimiza hitaji hili. Msamaha kamili wa dhambizilizopita, za sasa, na zijazo-na kufunguliwa kutoka katika mateso yote na adhabu walizozipata kuliahidiwa kwa wote ambao wangejiorodhesha katika vita vya kipapa vya kueneza utawala wake wa kidunia, kuwaadhibu maadui zake, au kuwaangamiza wale waliothubutu kukana ukuu wake wa kiroho. Watu walifundishwa pia kuwa kwa malipo ya fedha kwa kanisa wangeweza kujiweka huru kutoka katika dhambi na kuweka huru roho za rafiki zao waliokufa ambao walikuwa katika moto wa mateso. Kwa jinsi hii Rumi ilijaza hazina zake na kupata utukufu, anasa, na uovu wa wawakilishi wenye kujifanya, wa Yeye ambaye hakuwa na mahali pa kulaza kichwa chake.PLK 119.3

    Agizo la Kimaandiko la meza ya Bwana lilibadilishwa na kafara za miungu za misa. Makasisi walijifanya kuwa wanabadilisha mkate na mvinyo kuwa mwili na damu halisi ya Kristo. Kwa kiburi cha kukufuru walidai waziwazi kuwa na uwezo wa “kumuumba Mwumbaji wao.” Ili kuepuka kifo, Wakristo wote walitakiwa kukiri imani yao katika uzushi huu wa kutisha wenye kuitukana mbingu. Wale waliokataa walichomwa moto.PLK 120.1

    Adhuhuri ya Upapa ilikuwa ni usiku wa manane kwa maadili ya kidunia. Maandiko Matakatifu yalikaribia kutoeleweka, si tu kwa watu, bali pia kwa makasisi. Kama Mafarisayo wa zamani, viongozi wa kanisa walichukia nuru ambayo ingedhihirisha dhambi zao. Wakiwa wameondoa sheria ya Mungu, kipimo cha haki, walitumia mamlaka yasiyo na kikomo na kutenda uovu bila kuzuiwa. Dhuluma, uchoyo, na uasherati vilishamiri. Wala watu hawakurudi nyuma katika kutenda uhalifu wo wote ambao ungeweza kuwapa mali au cheo. Ikulu za mapapa na maaskofu zilikuwa ni eneo la ufisadi (zinaa, uasherati, ulevi) wa kuchukiza kuliko vyote. Baadhi ya mapapa waliotawala walikuwa na hatia za uhalifu wa kuchukiza kiasi kwamba watawala wa kiraia walijaribu kuwapindua hawa wenye vyeo vikuu kanisani wakiwa kama majitu ya kutisha maovu kiasi cha kutoweza kuvumiliwa kuendelea kukalia kiti cha enzi. Kwa kame kadhaa hapakuwapo na maendeleo katika kujifunza, sanaa, na ustaarabu. Kupooza kimaadili na kiakili kulianguka juu ya mataifa ya Kikristo.PLK 120.2

    Larger font
    Smaller font
    Copy
    Print
    Contents