Loading...
Larger font
Smaller font
Copy
Print
Contents
Tumaini la Vizazi Vyote - Contents
  • Results
  • Related
  • Featured
No results found for: "".
  • Weighted Relevancy
  • Content Sequence
  • Relevancy
  • Earliest First
  • Latest First
    Larger font
    Smaller font
    Copy
    Print
    Contents

    72 — Meza ya Bwana Yaanzishwa

    “Bwana Yesu, usiku ule aliotolewa, alitwaa mkate, naye akiisha kushukuru akaumega, akasema, Huu ndio mwiliwangu ulio kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu. Na vivi hivi baada ya kula akakitwaa kikombe, akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu; Fanyeni hivi kila mnywapo, kwa ukumbusho wangu. Maana kila mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata ajapo.” 1 Wakorintho 11:23-26.TVV 370.1

    Kristo, Mwana kondoo wa Mungu alikuwa karibu kukomesha desturi ya mifano na ibada za kafara, ambazo kwa muda wa miaka 4,000 zililenga kwa kifo chake, Pasaka, ambayo ilikuwa sikukuu ya taifa la Israeli, ilikuwa ifutika milele. Adhimisho la meza ya Bwana, ambalo Kristo alikuwa ameanzisha ndilo liadhimishwe na wafuasi Wake katika nchi zote na katika vizazi vyote.TVV 370.2

    Pasaka ilikuwa imeanzisha kuwa ukumbusho wa kukombolewa kwa Waisraeli kutoka katika utumwa wa Misri. Meza ya Bwana ilianzishwa kuwa ukumbusho wa kukombolewa kulikoletwa kama matokeo ya kifo cha, Kristo. Adhimisho la agizo hili ndiyo njia ya kutukumbusha daima kazi yake kuu kwa ajili ya wokovu wetu. Katika, nyakati za Kristo watu walikula Pasaka wakiwa katika hali ya kuketi kwa kuegemea. Wageni waliegemea kwenye kiti kirefu, kilichowekwa karibu na meza, mkono wa kulia ulikuwa huru uweze kutumika kula. Katika hali hiyo mtu aliweza kuegemea kichwa chake kifuani mwa yule aliyekaa karibu naye. Na miguu ilinyoshwa kando ilikuwa wazi kwa kutawadhwa na mtumishi aliyekuwa akitawadha kwa mzunguko upande wa nje ya mduara ule.TVV 370.3

    Kristo alikuwa angali kwenye meza ambapo chakula cha pasaka kilikuwa kimeandaliwa. Mikate isiyotiwa chachu ilikuwa mbele yake. Divai safi isiyochachu ilikuwako mezani. Vitu hivyo Kristo alivitumia kufananisha na kafara yake isiyo na kasoro. (Tazama 1 Petro 1:29.)TVV 370.4

    “Walipokuwa wakila, Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake, akasema, Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu. Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa akisema, Nyweni nyote katika hiki; kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi. Lakini nawaambieni, Sitakunywa kabisa tangu sasa uzao huu wa mzabibu, hata siku ile nitakapokunywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu.”TVV 371.1

    Yuda msaliti alipokea kutoka kwa Yesu mfano wa mwili wake uliovunjika na damu yake iliyomwagika. Msaliti akiwa ameketi mbele ya Mwana Kondoo wa Mungu alitafakari njama zake, na mawazo ya kutaka kisasi.TVV 371.2

    Wakati wa kutawadha miguu, Kristo alikuwa amedhihirisha kwa dhati kuwa anayafahamu mawazo ya Yuda. Alisema, “Si nyote mlio safi.” Yohana 13:11. Sasa Kristo akasema wazi Zaidi: “Sisemi habari za ninyi nyote, nawajua wale niliowachagua; lakini andiko lipate kutimizwa. Aliyekula chakula changu ameniinulia kisigino chake.”TVV 371.3

    Mpaka wakati huu wanafunzi walikuwa hawajamtilia shaka Yuda. Lakini walishikwa na wasiwasi, wakatazamia jambo fulani baya. Walipokuwa wakila katika hali ya ukimya, Yesu akasema, “Amin amin nawaambia, Mmoja wenu atanisaliti.” Fadhaa “ikawashika. Inawezekanaje mmoja wao, amsaliti hivyo Mwalimu wao Mtakatifu? Kumsaliti? Kwa nani? Hakika siye mmoja wa hawa wapendwa kumi na wawili!TVV 371.4

    Walipokumbuka jinsi maneno yake yalivyokuwa ya kweli, hofu na kutojiamini kukawashika. Kwa uchungu wa moyoni walianza kuuliza, mmoja mmoja, “Ni mimi, Bwana?” Lakini Yuda alikaa kimya. Hatimaye Yohana akauliza: “Bwana, ni nani?” Na Yesu akajibu, “Yeye aliyetia mkono wake pamoja nami katika kombe, ndiye atakayenisaliti.” Ukimya wa Yuda uliwaelekeza wote kwake. Kutokana na utata wa maswali na butwaa. Yuda hakuwa amesikia jibu la Yesu kwa swali la Yohana. Lakini sasa ili kukwepa uchunguzi wa wanafunzi, naye pia alimwuliza kama walivyo kuwa wameuliza “Ni mimi, Rabi?” Yesu akajibu kwa upole, “Wewe umesema.”TVV 371.5

    Kutokana na mshangao na utata wa kugunduliwa siri yake Yuda aliondoka haraka na kutoka. Kisha Yesu akamwambia “Uyatendayo yatende upesi .... Basi huyo akiisha kulipokea lile tonge, akatoka mara hiyo. Na kulikuwa ni usiku.”TVV 371.6

    Ulikuwa usiku wakati msaliti alipomuacha Kristo na kwenda katika giza kabisa. Mpaka kufikia hatua hii Yuda alikuwa hajavuka mpaka wa toba. Lakini alipoondoka na kumuacha Bwana wake na wanafunzi wenzake, alikuwa amevuka mpaka wa toba. Hakuna jambo la kumsaidia Yuda lilioachwa kufanywa. Hata baada ya kufanya mapatano mara mbili kumsaliti Bwana wake, Yesu bado alimpa nafasi ya kutubu. Kwa kusoma siri za makusudi ya msaliti, Kristo alimpa ushahidi wa dhati, wa Uungu wake. Huu ulikuwa mwito wa mwisho wa toba. Kutoka katika meza ya Bwana Yuda alienda zake ili kukamilisha kazi ya usaliti.TVV 372.1

    Katika kumtamkia ole Yuda, Kristo pia alikuwa na kusudi la rehema kwa wanafunzi wake. Alisema: “Nawaambia kabla hayajatukia, ili yatakapotukia mpate kuamini ya kuwa mimi ndiye.” Kama Yesu angalinya-maza, wanafunzi wangalifikiri kuwa Bwana wao hakuwa na uungu wa kujua mbele yatakayokuja, na hivyo alishtushwa. Mwaka mmoja uliopita Yesu alikuwa amewaambia wanafunzi wake kwamba aliwachagua watu kumi na wawili, lakini mmoja wao ni Shetani. Sasa maneno yake kwa Yuda yataimarisha imani ya wafuasi wake wa kweli wakati wa dhiki yake. Yuda atakapofikia mwisho wake wa kutisha, watakumbuka ole aliyosema juu ya msaliti.TVV 372.2

    Mwokozi alikuwa bado ana kusudi jingine. Wanafunzi walipaswa kutafakari jambo jingine kuhusu uvumilivu na rehema za Mungu, juu ya mtu mkosaji mkuu. Msaliti alikuwa amepata nafasi ya kushiriki meza ya Bwana, pamoja na Kristo. Kielelezo hicho ni kwa ajili yetu. Tunapomdhania mtu mmoja kuwa ni mkosaji na mwenye dhambi, haitupasi kumtenga, na kumwacha awe mateka kwa majaribu na kumsukumia, katika uwanja wa mapambano ya Shetani. Kristo aliwatawadha wanafunzi miguu yao kwa sababu walikuwa wakosefu na wenye dhambi, na hivyo wote wakafikishwa katika toba isipokuwa mmoja.TVV 372.3

    Larger font
    Smaller font
    Copy
    Print
    Contents